(Inatolewa chini ya Kanuni ya 99(9) ya kanuni za Bunge toleo la mwaka 2013)
1. UTANGULIZI
Mheshimiwa Spika,
Dira ya Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo ni “kuwa na
taifa lililohabarishwa vizuri, lina vijana wenye uwezo na malezi bora,
linathamini utamaduni wake na linakuwa mahiri katika michezo ifikapo
mwaka 2025.” Aidha, ‘dhamira’ ya wizara hii ni ‘kuendeleza utambulisho
wa taifa kwa kuwezesha upatikanaji mzuri wa habari, kuwawezesha vijana
kiuchumi na kukuza utamaduni na michezo kwa umma kwa maendeleo ya
kijamii na kiuchumi.’
Mheshimiwa Spika,
Kwa maoni ya Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, Serikali hii ya CCM
imeshindwa kutekeleza dira na dhamira iliyotajwa katika maandiko ya
kisera ya Wizara. Badala yake, chini ya usimamizi wa Wizara hii,
Tanzania imegeuka kuwa taifa lisilotaka watu kuhabarishwa vizuri juu ya
matendo ya watawala. Tanzania imegeuka kuwa taifa linalofungia magazeti
yanayofichua ufisadi, uchafu na matumizi mabaya ya madaraka miongoni
mwa viongozi, watendaji na watumishi wa Serikali hii ya CCM. Tanzania
imegeuka, chini ya usimamizi wa Wizara na Serikali hii ya CCM, kuwa
taifa linaloteka nyara wanahabari, kuwatesa kwa kuwang’oa kucha na
meno, kuwatoboa macho, kuwamwagia tindikali na hata kuwaua. Tanzania
sio nchi inayoandaa vijana wake tena. Haiwapi tena elimu bora wala
kuwapatia maarifa, uwezo na malezi bora; ni nchi isiyowawezesha wala
kuwathamini vijana wake; ni nchi inayoruhusu vijana wake kunyonywa na
kutoendelezwa; na ni taifa ambalo limeachia utamaduni utambulisho wake
kama taifa kupotea kabisa. Aidha, katika fani ya michezo ya aina zote,
Tanzania imeporomoka kutoka taifa lililokuwa linaheshimika kimataifa
katika miaka ya sabini na kuwa alichokiita rais mstaafu Ali Hassan
Mwinyi, ‘kichwa cha mwendawazimu’ ambacho kila kinyozi anajifunzia
kunyolea!
2. UHURU WA UHARIRI NA USALAMA WA WANAHABARI
Mheshimiwa Spika,
Kwa masikitiko makubwa, Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inalitaarifu
Bunge lako tukufu kwamba sasa Tanzania imeingia rasmi katika orodha ya
fedheha (The List of Shame) ya mataifa ambayo taaluma ya habari ni
taaluma ya hatari kwa wale wote wanaoitumia kama sehemu ya wajibu wao
kwa taifa na kama ajira yao. Kwa mujibu wa taarifa ya Kamati ya Kulinda
Waandishi wa Habari Ulimwenguni (the Committee to Protect Journalists -
CPJ) iliyotolewa mwaka huu 2013, kwa mara ya kwanza tangu kuanzishwa
kwa CPJ mwaka 1992, Tanzania imeingizwa kwenye orodha ya nchi 20 ambazo
ni hatari kwa waandishi wa habari kufanya kazi zao kutokana na hatari
ya kuuwawa kwa mwaka 2012 (20 Deadliest Countries in 2012). Kwa mujibu
wa taarifa hiyo, ilishikilia nafasi ya 7 ulimwenguni kati ya nchi 20
zinazoongoza kwa kuhatarisha maisha ya waandishi wa habari.