Na Thobis Mgimwa a.k.a Mr Tee Kilaka Mashine
Mbeya ni miongoni mwa mikoa yenye hazina kubwa ya vipaji vya muziki nchini Tanzania. Kutoka kwa wasanii wa Hip Hop, Bongo Fleva, RnB hadi muziki wa asili, vipaji vinavyochipuka havina ukomo. Lakini changamoto kubwa imekuwa wazi: ni kwanini wasanii hawa licha ya uwezo wao mkubwa hawafanikiwi kufika mbali? Je, tatizo ni vipaji, mazingira au mfumo wa muziki? Ukweli ni kwamba “Mawazo tu” ndiyo yanayowakwamisha wengi.
Hapa chini naeleza sababu kuu zinazokwamisha wasanii wa Mbeya, hata
wale waliobarikiwa na vipaji vya kipekee.
MASHINDANO MAKALI KATIKA SOKO LA MUZIKI
Kwa sasa soko la muziki nchini na duniani limejaa ushindani mkubwa.
Kila siku wasanii wapya wanazaliwa na wale waliotangulia wanaendelea
kujiimarisha kupitia kampuni kubwa, usimamizi bora na mitandao ya kisasa ya usambazaji.
Hali hii huwafanya wasanii wa mikoa kama Mbeya kukabiliwa na kazi ngumu ya
kujitambulisha bila kuwa na mtandao imara wa msaada wa kitaaluma.
MABADILIKO YA TEKNOLOJIA
Teknolojia imebadilisha sana mchezo wa muziki. Kutoka CD hadi
streaming platforms kama Spotify, Apple Music, Boomplay na YouTube. Ingawa hizi
ni fursa, kwa wasanii wa Mbeya ambazo hawana maarifa ya kidigitali, zinageuka
kuwa kikwazo kikubwa. Bila kuelewa mbinu za kujiweka mtandaoni, muziki wao
hubaki kusikika ndani ya mtaa pekee.
MASOKO NA MIKAKATI YA KUJITANGAZA
Mafanikio ya msanii si tu kutegemea kipaji, bali pia namna anavyoweza
kujitangaza. Wasanii wengi hawana bajeti wala elimu ya kutosha ya masoko —
matokeo yake wanashindwa kueneza kazi zao nje ya miduara midogo ya marafiki.
Bila kujifunza mbinu bora za digital marketing, hata kazi bora zaidi zinaweza
kupotelea hewani bila kutambulika.
USHIRIKIANO NA WASHIRIKA WA MUZIKI
Hakuna msanii anayeweza kusimama peke yake. Mafanikio yanahitaji timu
— kuanzia kwa watayarishaji, waandishi wa nyimbo, wasambazaji, hadi mameneja.
Mara nyingi wasanii wa Mbeya hukosa mitandao ya kushirikiana ambayo ingeweza
kuwakutanisha na fursa kubwa za kitaifa au kimataifa. Kukosa ushirikiano ni
sawa na kujifungia kwenye chumba bila mlango wa kutokea.
MABADILIKO YA LADHA ZA WASIKILIZAJI
Ladha ya muziki inabadilika kila wakati. Wakati mwingine msanii
anaweza kuwa na mtindo wa kipekee lakini usioendana na kile ambacho
wasikilizaji wanataka kwa wakati huo. Kujifunza kuendana na mabadiliko haya ni
sanaa yenyewe. Msanii anapaswa kuwa tayari kujifunza, kubadilika na kufanyia
kazi mrejesho wa mashabiki.
MTAZAMO WA WASANII WENYEWE
Wakati mwingine changamoto kuu haipo nje, bali ndani ya fikra za
msanii. Wengi huamini kuwa kipaji pekee kinatosha kufanikisha ndoto zao. Lakini
muziki ni biashara — unahitaji nidhamu, ufuatiliaji wa masoko, kujifunza
usimamizi wa fedha, mahusiano mazuri na mashabiki pamoja na kuwa na maono ya
mbali. Bila haya, kipaji hubaki kuwa hadithi isiyosimuliwa.
MITANDAO YA KIJAMII NA KUJENGA BRAND BINAFSI
Katika dunia ya sasa, msanii anayeweza kutumia vyema Instagram, TikTok, Facebook na YouTube ana nafasi ya kujenga jina lake haraka kuliko kusubiri kampuni kubwa imtambue. Lakini wengi wanatumia mitandao kwa burudani tu badala ya kuikuza kama jukwaa la kazi zao. Brand ya msanii hujengwa mtandaoni kabla hata ya muziki kusikika.
Mafanikio ya msanii wa muziki hayategemei kipaji peke yake bali
mchanganyiko wa juhudi, maarifa ya soko, ushirikiano na mtazamo wa kibiashara.
Wasanii wa Mbeya wana hazina kubwa ya vipaji, lakini “mawazo tu” — namna
wanavyojiona, wanavyopanga na wanavyotumia fursa — ndicho kinachowakwamisha.
WITO KWA WASANII
Ni muda wa kubadilika.
Ni muda wa kujifunza.
Ni muda wa kufungua mawazo.
KILIO CHA VIPAJI
KUTOKA MBEYA KUFIKA MBALI, KIKO KWENYE MAWAZO!
Respect kwenu
ReplyDelete