Wednesday, 5 March 2025

DNASSE AFUNGUKA KUHUSU SAFARI YAKE YA MUZIKI NA MUSTAKABALI WA WASANII WA NYANDA ZA JUU KUSINI

Katika mahojiano maalum na Burudani Mbeya Media, mwanamuziki wa kizazi kipya DNasse kutoka mkoa wa Songwe amefunguka kuhusu safari yake ya muziki, changamoto alizokutana nazo, mafanikio aliyoyapata, na mtazamo wake kuhusu maendeleo ya muziki katika ukanda wa Nyanda za Juu Kusini.

SAFARI YA KUINGIA KWENYE MUZIKI

DNasse alieleza kuwa mapenzi yake kwa muziki yalianza tangu

utotoni, lakini aliamua kuingia rasmi katika fani hii alipoona fursa zilizopo kwenye tasnia ya muziki. Kazi yake ya kwanza kurekodi ilikuwa wimbo uitwao Muda Mrefu, ambao hata hivyo haukufanikiwa kutoka rasmi.

Wimbo wake wa kwanza kusikika kwenye vyombo vya habari ulikuwa Rangi Yako, ambao ulimpatia nafasi kubwa ya kukutana na watu mbalimbali na kuanzisha rasmi safari yake ya muziki. DNasse anasisitiza kuwa msanii anahitaji kuwa na management ili kurahisisha kazi yake, kuhakikisha usambazaji wa kazi, kufanya promotion, kutafuta masoko na shows, huku msanii akibaki na jukumu la kubuni na kuendeleza kipaji chake.

MAFANIKIO NA CHANGAMOTO

Wimbo wake wa Nitatoaboa ulimfungulia milango na kumfanya ajulikane zaidi, huku ukichezwa kwenye vyombo mbalimbali vya habari. Hadi sasa, DNasse ameshatoa zaidi ya nyimbo kumi, pamoja na nyimbo tano zinazohusu masuala ya kijamii.

Hata hivyo, amekutana na changamoto nyingi, kama

vile ugumu wa kufikisha kazi zake sokoni kwa wakati, lakini changamoto hizi zimemjenga kwa kumfanya awe na nidhamu na kutoridhika kirahisi. Anasisitiza kuwa nidhamu na heshima ni nguzo muhimu kwa msanii kufanikisha ndoto zake.

SOKO LA MUZIKI WA NYANDA ZA JUU KUSINI

Kwa mujibu wa DNasse, wasanii wengi wa Nyanda za Juu Kusini wanapokaribia kuingia kwenye mainstream ya muziki Tanzania, wanashindwa kudumu kutokana na changamoto kama nidhamu duni, kukosa usimamizi mzuri, kutokuwa na wawekezaji wa kutosha, na kujisahau wanapoanza kupata mafanikio.

Anapendekeza kuwa vyombo vya habari vya ukanda huu viongeze juhudi katika

kusaidia wasanii wa hapa kwa kuandaa mpango maalum vya kuutangaza muziki wao na kushirikiana na wasanii katika matukio mbalimbali. Pia anawashauri wawekezaji kuwa na imani zaidi na wasanii ili kuendeleza vipaji vyao.

MATARAJIO YA BAADAYE

DNasse tayari ametoa EP yake iliyopewa jina Ngoma Droo yenye nyimbo New Face na One Day na kwa sasa anafanya maandalizi ya kutoa albamu yake ya kwanza. Katika ndoto zake, anataka kuwa alama kwenye muziki wa Tanzania na kuandikwa kwenye historia kupitia kazi zake.

Akiwa tayari amefanya kazi na Nay wa Mitego, DNasse anatamani kufanya kazi na Young Lunya. Mbali na muziki, pia anajishughulisha na kilimo na biashara ndogondogo za kujiingizia kipato.

Katika ujumbe wake kwa vijana wanaojitafuta kimaisha, anawashauri kuwa na nidhamu na heshima kwa muda, fedha, watu, na kazi wanazofanya, kwani hizi ndizo nguzo za mafanikio.

HITIMISHO

DNasse anaendelea kutamba katika muziki wa kizazi kipya, akiwa mmoja wa wasanii wanaopeperusha bendera ya Nyanda za Juu Kusini. Kwa juhudi zake na maono makubwa aliyonayo, ana nafasi kubwa ya kufikia mafanikio makubwa zaidi kwenye tasnia ya muziki Tanzania. Mashabiki wake wanapaswa kuendelea kumfuatilia kwani bado ana mengi ya kuonesha!


0 comments:

Post a Comment